Monday, March 26, 2012

Ifahamu Tanzania


 Na Goustone Isole

Hifadhi za Taifa Tanzania

Ramani ya Tanzania
Tanzania ni moja kati ya nchi tano zinazounda Jumuiya ya Afrika Mashariki. Nchi hii ipo upande wa Mashariki kabisa mwa bara la pili kwa ukubwa duniani baada ya lile la Asia, Afrika. Nchi hii kwa upande wa Mashariki imepakana na bahari ya Hindi.
Mlima Kilimanjaro
Nchi ya Tanzania inasifika ulimwenguni kutokana na vivutio vingi, vikijumuisha vya asili na kihistoria. Vivutio vya asili ni vile ambavyo vimekuwapo tangu enzi na enzi kwa mfano mbuga za wanyama, milima na maziwa makubwa. Tanzania inasifika kwa kuwa na mbuga kubwa za wanyama wa porini kama vile Serengeti na Ngorongoro. Kwa upande wa milima, kuna mlima Kilimanjaro, Mlima mrefu kuliko yote barani Afrika, upatikanao mkoa wa Kilimanjaro uliopo karibu na uwanja wa ndege wa kimataifa wa Kilimanjaro, Kilimanjaro International Airport (KIA). Pia kuna milima ya Usambara, Mlima Meru na mengine mingi ambayo pia makazi ya wanyama wa porini pamoja na ndege wa aina mbalimbali. Maziwa maarufu yapatikanayo nchini Tanzania ni Ziwa Victoria, ziwa kubwa kuliko yote barani Afrika, ziwa Tanganyika, ziwa lenye kina kirefu kuliko yote barani Afrika bila kusahau ziwa Nyasa.
Simba akiwa mbugani, Serengeti
Kondoa- Irangi
Vivutio vya kihistoria ni vile ambavyo vimekuwa vikijitokeza kutokana hatua ambazo mwanadamu amekuwa akizipitia kufikia maendeleo. Mfano mzuri, ni ile michoro ya mapangoni inayopatikana katika mji mkuu wa Tanzania, Dodoma. Michoro hii inapatikana katika mji mmoja maarufu ujulikanao kama Kondoa- Irangi. Si hivyo tu, kuna vivutio vingi tu vya kihistoria kama vile sehemu ambazo mwanadamu wa kale alianza uvumbuzi wa chuma.



Tanzania na Utalii

Nchi ya Tanzania imekuwa ikifaidika kutokana na vivutio vya utalii. Kila mwaka idadi ya watalii kutoka sehemu mbalimbali duniani imekuwa ikifika nchini Tanzania kujionea vivutio hivi pamoja na maajabu yanayopatikana katika nchi hii. Mojawapo kati ya maajabu ambalo limekuwa likijipatia umaarufu kila kukicha ni ile hali ya wanyama wa mwituni kuishi pamoja na binadamu katika hifadhi ya Ngorongoro. Uwepo wa watalii ndani ya Tanzania umesaidia sana upatikanaji wa fedha za kigeni na pia umekuwa chachu ya nchi hii kutambulika kimataifa.
Hotel ya Kitalii
Utalii pia umechangia maendeleo ya sekta nyingine kama vile usafirishaji na biashara kwani kumekuwepo ujenzi wa barabara katika viwango vya lami hasa katika maeneo yenye vivutio vya kitalii, ujenzi wa mahoteli makubwa kama ilivyo katika mji wa kitalii, Arusha, maarufu kama Geneva ya Afrika.
Ni jambo la msingi kwa watanzania kuvilinda na kuviheshimu vivutio hivi kwani vimekuwa msaada mkubwa hasa katika suala la maendeleo. Kutokana na pesa zinazotokana na utalii, nchi ya Tanzania imeweza kufanya mambo ya kimaendeleo kama vile nilivyoonesha hapo awali na pia imesaidia ujenzi wa mashule na pia hospitali karibu kwa kila kata nchi nzima.



Hali ya Utalii wa Ndani nchini Tanzania (Domestic Tourism)

Utalii wa ndani katika nchi ya Tanzania umekuwa si wa kuridhisha japokuwa kumekuwepo hamasa kutoka kwa mamlaka ya hifadhi za Tanzania maarufu kama Tanapa. Hamasa hizi ni kama vile kuwatoza wazawa fedha kidogo. Hii bado haijasaidia kushinikiza utalii wa ndani. Ni wazi wengi wa watanzania hawajafahamu nini maana ya utalii na cha ajabu ni kwamba hawajachukua hata nafasi ya kujiuliza ni kwa nini wageni kutoka nje hufika nchini mwetu kuja kushuhudia vivutio hivi.
Watalii wa Nje
Ni wazi sasa baada ya kuyasoma yote hapo juu, utahamasika na kufikiria kutembelea moja ama baadhi ya hifadhi zipatikanazo hapa nchini Tanzania na pia kushiriki vyema katika kuhakikisha tunazihadhi ipasavyo hifadhi zetu.
Kufahamu hifadhi zipatikanazo nchini Tanzania, bonyeza hapa.

Kufahamu jinsi Shirika la hifadhi za Taifa linavyofanya kazi na jinsi ya kutembelea mbuga za wanyama pamoja na vivutio vingine, Bonyeza hapa ku-download **('PDF' file in English (UK)**.
Kurudi juu, bonyeza hapa

No comments:

Pageviews past week